Sunday, November 28, 2010

RADIO UPLANDS YAFANYA TAMASHA KUTIMIZA MIAKA MITATU YA HABARI NA BURUDANI

MIAKA MITATU YA UPLANDS FM RADIO(NJOMBE).

Tamasha la kutimiza kwa miaka mitatu ya Radio Uplands Fm katika mkoa wa Njombe walayai hapa linafanyika leo katika viwanja vya saba saba mchana baadae kufuatia na shoo ya muziki katika ukumbi wa Vegas uliopo mjini hapa.

Akiongea na mtandao huu kwa kwa nyakati tofauti Meneja wa radio hiyo ya Uplands Fm bwana Vitus Swale amesema kuwa tamasha hilo litaanza mnamo saa tatu asubuhi,ambapo kutakuwa na michezo mbali mbali katika viwanja hivyo vya saba saba.

Amesema kuwa baadhi ya mambo yatakayokuwepo uwanjani hapo ni pamoja na mchezo wa mpira wa miguu,ambao utawakutanisha timu ya mpira wa miguu ya Uplands Fm na Chuo cha ualimu Hagafiro kilichopo wilayani njombe.

Pia ameongeza kuwa mbali na mchezo wa kandanda pia kutakuwa na mchezo wa mpira wa pete kwa wasichana,mpira wa wavu,kukimbia na hata kuvuta kamba.

Mbali na mashindano hayo pia kutakuwa na bendi na vikundi mbali mbali vya muziki ambapo vijana wa kizazi kipya kutoka wilayani hapa wataongozwa na mwanamuziki kutoka jijini dar es salaam BELLE 9 anayetamba na nyimbo zake za MASOGANGE,WE NI WANGU NA LADHA YA MAPENZI.

Katika kuadhimisha miaka hiyo mitatu kituo hicho cha radio cha Uplands Fm kitasoma risala yake toka kuanzishwa kwake hadi kufanikiwa kutimiza miaka mitatu leo siku ya tarehe 28 mwezi huu wa kumi na moja,mbali na risala hiyo itakayosomwa mbele ya mgeni rasmi katika shughuli hiyo mkuu wa wilaya ya Njombe Bi. SARA DUMBA pia zitasomwa risala za wadau wa radio kutoka sehemu mbali mbali.

Wakizungumza na mtandao huu baadhi ya wakazi wa wilaya ya Njombe wamesema kuwa toka kuanzishwa kwa radio ya Upland mkoani hapa Njombe,imewasaidia kwa kiasi kikubwa kwa kuwahabarisha na hata kuwaburudisha kwa vipindi mbali mbali vya habari na burudani vinavyorushwa na kituo hicho cha radio mkoani hapa.

Na miongoni mwa watangazi na waandishi wa kituo hicho ni pamoja na ASIFIWE NGAO(MSIMAMIZI WA VIPINDI),SHABANI LUPA(MHARIRI MKUU),FESTUS PANGANI,(MTANGAZAJI,MWANDISHI),HAMISI KASAPA(MTANGAZAJI MWANDISHI),BENNY NGINDO (MTANGAZI,PRODUCER),SARA MANDE(MTANGAZAJI),CONSOLATA KIOMBO(MTANGAZAJI),GABRIEL KILAMLYA(MWANDISHI),SHEDRACK MWANSASU(MTANGAZAJI)BRAISON MGOJI(MTANGAZAJI),DAVID JOTHAM(MTANGAZAJI).

Sherehe hizo za kutimiza miaka mitatu zitafanyika katika viwanja vya saba saba wilayani njombe.

Friday, November 26, 2010

NJAA YASUMBUA WAKAZI WAKATA YA NDULI MKOANI IRINGA.

WALIHAIDIWA KUPEWA CHAKULA CHA
MSAADA NA WAGOMBEA WAO.

Wananchi wa kata mpya ya Nduli katika Manispaa ya Iringa wameomba kupatiwa chakula cha msaada kutokana na njaa kali inayowakabili kwa madai kuwa tangu waiombe serikali iwapatie msaada huo, hawajawahi kusaidiwa.

Imedaiwa kuwa Wananchi hao wamekuwa wakila mlo mmoja kwa siku na wanafunzi wa shule za msingi wameathirika zaidi kwa kuwa shule nyingi hazina uwezo wa kuwaandalia wanafunzi chakula cha mchana hali inayopelekea kutokuwa na isikivu wa kutosha wanapokuwa darasani.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Nduli, Ayubu Mwenda alisema tatizo la chakula limekuwa kubwa, kutokana na mazao mengi kukauka kabla ya kukomaa kufuatia ukame ulioathiri kata yao.

Amesema tatizo hilo, limeshusha kwa kiasi kikubwa kiwango cha wanafunzi kufaulu kwa madai kuwa wengi wao wamekuwa wakienda shule bila kula chochote hadi jioni wanaporejea nyumbani.

Wananachi hao walisema kuwa wakati wa kampeni, waliahidiwa kupewa chakula na wagombea wao, lakini bado hawajakumbukwa jambo ambalo linawafanya waanze kukosa imani na viongozi waliowaweka madarakani.

Kwa upande wake diwani mpya wa Kata ya Nduli, aliahidi kutoa chakula cha msaada kwa ajili ya wanafunzi wa maeneo ya kata hiyo mara shule itakapofunguliwa na kwamba hivi sasa hawezi kutokana na ukweli kwamba bado hawajaanza kazi.

Takwimu za awali zilizotolewa na Halmashauri ya Wilaya ya Iringa wakati kata hiyo haijahamishiwa katika Halmshauri ya Manispaa, zinaonyesha kuwa zaidi ya watu 13,000 wanakabiliwa na tatizo la njaa katika kata hiyo.

Thursday, November 25, 2010

NAIBU WAZIRI WA MAJI AWEKA AWEKA MIPANGO YAKE KATIKA KUTATUA KERO ZA MAJI.

NAIBU WAZIRI WA MAJI AWEKA AWEKA MIPANGO YAKE KATIKA
KUTATUA KERO ZA MAJI.


Siku Moja Baada ya kuteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Maji Katika Baraza Jipya La Mawaziri lililotangazwa Hapo tarehe 24 mwezi wa 11 mwaka wa 2010 Mbunge Mteule wa Njombe Magharibi Mhandisi Gerson Lwenge Ameweka Bayana Mipango yake katika kutatua Kero za Maji Wilayani Njombe.

Akizungumza na mtandao huu kwa njia ya simu Mchana leo Mhandisi Lwenge Amesema Baada ya kuteuliwa Kuwa Naibu Waziri wa Maji Wanategemea kuandaa mpango Mkakati wa kuboresha Miundombinu ya maji hatua ambayo amesema itasaidia kupunguza Kero hizo bila kusahau wakazi wa mkoa wa njombe ambako ndiko alikopata kura zilizomfikisha hapo alipo katika wizara hiyo kama naibu waziri.

Naibu Waziri huyo Amesema kwa kushirikiana na Mbunge wa Njombe Kusini Ambae pia ni Spika wa Bunge la Jamuhuri wa Muungano wa Tanzania Bi Anna Makinda wanategemea kuunganisha nguvu zao ili kuweza kutatua Matatizo ya Wananchi wa Mkoa mpya wa Njombe kwa ukaribu na kuahidi kufanya kazi kwa ushirikiano.

Amesema kwa Wilaya ya Njombe kufanikiwa kupata Mawaziri Wawili katika Baraza la Mawaziri ni hatua ya kihistoria ya kuelekea kutatuliwa kwa Kero na Matatizo mbalimbali ya Wakaazi wake na hiyo inaonyesha kwamba kuna watu wenye uwezo waliopo katika mkoa huu wa Njombe ambao ni mkoa moya na tayari umeishatoa viongozi wa ngazi za juu katika serikali ya Jamuhuri wa Muungano wa Tanzania,na hivyo ni hatua ya kujivunia kwa wananchi wa mkoa huu wa njombe kwa kuweza kuwa na viongozi wa ngazi za juu kabisa seriukalini na hivyo wao kama viongozi ni jukumu lao kuwatumikia wananchi hao wa mkoa huo wa njombe.

Hata hivyo Mheshimiwa Lwenge amesema licha ya kuwa sasa yeye ni naibu waziri lakini sit u ni kwa wananchi wa mkoa huo wa njombe bali pia ni kwa wananchi wa Tanzania kwa ujumla ikizingatiwa kuwa yeye ndiye naibu waziri hivyo atakuwa na kazi kubwa ya kumpa Waziri wake katika wizara hiyo yale yote yanayotokea nchini katika wizara yake.

Akizungumzia Sura ya Baraza Zima la Mawaziri ambalo limejumuisha Mawaziri Takribani 24 Wapya na Wengine Tisa wa Zamani wakikosa Nafasi Mhandisi Lwenge Amesema Hakuna Ulazima kwa kila Mbunge kuwa Waziri bali anaweza kushiriki Shughuli za Serikali kupitia Idara Tofauti Ndani ya Bunge

Amesema kwa Yoyote aliefanikiwa kuwa Mbunge Angeweza Kuwa Waziri katika Wizara yoyote lakini kwa wale walioteuliwa ni kama Wawakilishi wa Watanzania huku akiahidi kutekeleza yale yote alioyahaidi katika Siku 71 za Kampeni

Pia ameongeza kuwa kwa wale ambao hawakuwa mawaziri wanayo nafasi ya kutoa matatizo yao katika bunge la jamuhuri ya muungano na hivyo isingekuwa rahisi kwa wote kuwa mawaziri hivyo kinachohitajika ni kushirikiana kwa lengo la kupeleka mbele taifa la Tanzania.

Aidha Naibu Waziri Lwenge Amesema Hoja zinazozushwa na Baadhi ya Wanasiasa kuhusu umuhimu wa Baadhi ya Wizara Amesema Hoja hizo Hazina uzito Kwani kila Wizara Ina Umuhimu wake Kwenye Jamii.

Mapema Asubuhi Leo Katibu Mkuu wa CHADEMA Dr Wilbroad Slaa alinukuliwa na Moja ya Chombo cha Habari akisema kuwa Baadhi ya Wizara Hazina Umuhimu na kudai kuwa Zimeundwa ili kuwafurahisha Watu Fulani na kuitaja Wizara ya Utumishi wa Umma kuwa haina Umuhimu.

KUBADILIKA KWA MITAALA YA ELIMU MARA KWA MARA KUNAONGEZA KUSHUKA KWA ELIMU NJOMBE.

KUBADILIKA KWA MITAALA YA ELIMU MARA KWA MARA KUNAONGEZA KUSHUKA KWA ELIMU NJOMBE.


Tabia ya Serikali ya kubadilishabadilisha Mitaala mara kwa mara katika Shule za Msingi na Sekondari imeelezewa kuwa Sababu Mojawapo inayochangia kuporomoka Kwa Kiwango cha Elimu Wilayani Njombe

Hatua Hio pia imesababisha kuendelea kwa Tatizo la Upungufu wa Vitabu katika Shule za Msingi kwani Shule hulazimika kununua Vitabu Vipya kila Mtaala unapobadilika hali ambayo shule nyingi hazina Uwezo huo

Wakizungumza na mtandao huu katika Maadhimisho ya Wiki ya Vitabu Nchini katika Maktaba ya Wilaya ya Njombe Baadhi ya Wadau wa Elimu Wamesema Kila Wakati Serikali inapobadilisha Mitaala husababisha kuongezeka kwa Tatizo la Vitabu kwani Vile vilivyonunuliwa Awali Havitumiki Tena katika mitaala hiyo mipya.

Wamesema Tatizo Nyinyine linalosababisha kuendelea kwa Tatizo la Vitabu kwenye Shule za Msingi ni upungufu wa Fedha ya Ruzuku inayotolewa na Serikali kupitia Mradi wa MMEM ambao haukidhi mahitaji ya Shule zote

Kwa Mujibu wa Takwimu za Wilaya ya Njombe Yenye Jumla ya Shule 181 ni Shule sita Tu Ndio Zenye Maktaba ambazo pia Zinakabiliwa na Upungufu wa Vitabu

Takwimu hizo za Hali ya Upatikanaji Vitabu katika Shule Hizo zinaonesha kuwa kutokana na Idadi ya Wanafunzi Sabini na Sita Elfu,Mia Tatu Sitini na Sita wanafunzi Watatu hulazimika kuchangia Kitabu Kimoja kitu kinachopelekea kurudishwa nyuma kitaaluma.

WATENDAJI KATIKA SEKTA YA AFYA MKOANI IRINGA WASHAURIWA KUBORESHA HUDUMA.

WATENDAJI KATIKA SEKTA YA AFYA MKOANI IRINGA WASHAURIWA KUBORESHA HUDUMA.



Mganga Mkuu wa Mkoa wa Iringa Dokta Ezekiel Mpuya Amewaelekeza Watendaji wa Afya katika Halmashauri za Manispaa Mkoani Humo kubadili Mtazamo wao katika kufanyamaamuzi ya Rasilimali Watu kwa Lengo la Kuboresha Utolewaji wa huduma za Afya kwa Wananchi

Dokta Mpuya alikuwa akizngumza na Watendaji hao wa Afya Waliokutana Mjini Iringa Katika mafunzo ya Menejimeni ya Rasilimali Watu yaliokusudia Kuboresha Huduma za Afya Mkoani Iringa.

Akizungumza katika Mafunzo hayo Mganga huyo Amesema sekta ya Afya Mkoani Iringa ni Moja ya Sekta Zinazokabiliwa na Changamoto Mbalimbali ikiwemo upungufu wa Rasilimali watu hususani Maeneo ya Vijijini hali ambayo husababisha Misongamano ya Watu katika Vituo vya Afya na Zahanati hali ambayo husababisha Malalamiko kutoka kwa Wananchi.

Kwa Upande wao Madaktari wanaoshiriki katika Mafunzo hayo kutoka Wilayani Njombe wamesema Njia pekee kwa Serikali kuboresha Huduma ni kuongeza Vitendea kazi pamoja na kuongeza Motisha kwa Wafanyakazi katika sekta hiyo.

Wednesday, November 24, 2010

BALAZA JIPYA LA MAWAZIRI HILI HAPA KUWATUMIKIA WANANCHI

BALAZA JIPYA LA MAWAZIRI HILI HAPA
KUWATUMIKIA WANANCHI


Hili ndilo balaza letu jipya la Mawaziri hili hapa kuwatumikia wananchi wa tanzania kwa ujumla,tunatumaini kuwa litakuwa ni balaza lenye tija kwa Taifa kwa ujumla...

Ona hapa...


1. Ofisi ya Makamu wa Rais – ( Muungano) Samia Suluhu

2. Ofisi ya Makamu wa Rais – (Mazingira) Dr. Terezya Luoga Hovisa

4. Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge): William Lukuvi

2. Uwekezaji na Uwezeshaji Dr. Mary Nagu

5. Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) George Huruma Mkuchika

Naibu: Aggrey Mwanri

Naibu: Kassim Majaliwa

6. Wizara ya Fedha Mustapha Mkulo

Naibu: Gregory Teu

NAibu: Pereira Ame Silima

7. Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Shamsi Vuai Nahodha

Naibu: Balozi Khamis Suedi Kagasheki

8. Wizara ya Katiba na Sheria Celina Kombani

9. Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Bernard K. Membe Naibu: Mahadhi Juma Mahadhi

10. Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Dr. Hussein Ali Hassan Mwinyi

11. Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi Dr. Mathayo David Mathayo

Naibu: Benedict Ole Nangoro

12. Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Naibu: Charles Kitwanga

13. Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Prof. Anna Tibaijuka Naibu: Goodluck Ole Madeye

14. Wizara ya Maliasili na Utalii Ezekiel Maige

15. Wizara ya Nishati na Madini William Mganga Ngeleja 1. Adam Kigoma Malima

16. Wizara ya Ujenzi Dr. John Pombe Magufuli

Naibu: Dr. Harrison Mwakyembe

17. Wizara ya Uchukuzi Omari Nundu

Naibu: Athumani Mfutakamba

18. Wizara ya Viwanda na Biashara Dr. Cyril Chami

Naibu: Lazaro Nyalandu

19. Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Dr. Shukuru Kawambwa

Naibu: Philipo Mulugo

20. Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii Dr. Haji Hussein Mpanda

Naibu: Dr. Lucy Nkya

21. Wizara ya Kazi na Ajira Gaudensia Kabaka Makongoro Mahanga

22. Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto Sophia Simba Umi Ali Mwalimu

23. Wizara ya Habari, Vijana na Michezo Emmanuel John Nchimbi

Naibu Waziri. Fenella Mukangara

24. Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki Samuel John Sitta

Naibu Dr. Abdallah Juma Abdallah

25. Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika Prof. Jumanne Maghembe

Naibu: Christopher Chiza

26. Wizara ya Maji: Prof. Mark James Mwandosya


27. Ofisi ya Rais (Utawala Bora) Mathias Chikawe

Ofisi ya Rais – Mahusiano na Uratibu: Stephen Wassira

28.Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma Hawa Ghasia

FINCA TANZANIA WAWASHAURI WANANCHI KUTOJISAAHAU NA MIKOPO WANAYOPATA

FINCA TANZANIA WAWASHAURI WANANCHI KUTOJISAAHAU
NA MIKOPO WANAYOPATA

Wafanyabiashara mbalimbali wilayani Njombe Mkoani Iringa wametakiwa kutojisahau pindi wanapopata mikopo kwenye mashirika mbalimbali yanayotoa mikopo hiyo ili kuboresha biashara zao na kujikwamua na umaskini.

Hayo yamesemwa na Meneja wa shirika la mikopo la FINCA TANZANIA LIMITED tawi la Njombe Bwana Binnah Wakibara wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake.

Bwana Wakibara amesema kuwa shirika lake linatoa mikopo kwa njia mbili ambapo ni kupitia vikundi au mtu binafsi na kuongeza kuwa mkopo huo ni kwa ajili ya kuendeleza na kukuza biashara na siyo kuanzishia au kufanyia shughuli nyingine tofauti.

Akieleza changamoto walizokutana nazo tangu kuanzishwa kwa tawi hilo mjini Njombe mwaka 2005,amesema kuwa baadhi ya watu waliofanikiwa kuchukua mikopo hiyo wamekuwa wakishindwa kulipa marejesho katika wakati unaotakiwa kutokana na kuyumba kwa biashara zao au baadhi ya wateja kuchukua mikopo binafsi ambapo hushindwa kurejesha kwa wakati.

Aidha amewataka wananchi wa Njombe ambao ni wajasiliamali kutoogopa kufika ofisini kupata maelezo namna ya kupata mkopo huo na kuongeza kuwa FINCA ni kwa ajili ya kukuza kipato cha mfanyabiashara na kwamba masharti ya mikopo hiyo ni nafuu.

WATAKIWA KUPIMA AFYA ZAO NJOMBE MKOANI IRINGA

WAHUDUMU WA NYUMBA ZA KULALA WAGENI NA WAHUDUMU
MBALI MBALI WATAKIWA KUPIMA AFYA ZAO.


Wahudumu wa nyumba za kulala wageni (GUEST HOUSE) na wahudumu wa saloon za kike na za kiume wilayani Njombe Mkoani Iringa wametakiwa kujitokeza kupima afya zao badala ya kusubiri kukamatwa na maafisa wa afya.

Hayo yamebainishwa na Afisa afya wa halmashauri ya mji wa Njombe BI.Saada Milanzi akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake juu ya umuhimu wa utunzaji wa mazingira.

Akisoma kifungu cha sheria ya afya cha mwaka 2009 Bi.Milanzi amesema kuwa kifungu hicho kinawataka wafanyabiashara wote wa vyakula,wahudumu wa saloon na wahudumu wa nyumba za kulala wageni wanatakiwa kupima afya zao kila baada ya miezi sita lakini matokeo yake wahusika hao wamekuwa wakikaidi sheria hiyo.

Akieleza baadhi ya changamoto wanazokumbana nazo katika utendaji wa kazi amesema kuwa hospitali na zahanati za halmashauri ya mji wa Njombe zinakabiliwa na upungufu wa maafisa wa afya hali inayopelekea kushindwa kuwafikia wananchi wote kuwapa elimu juu ya utunzaji wa mazingira.

Katika hatua nyingine amezitaja baadhi ya adhabu ambazo zimekuwa zikitolewa n kwa wanaoshikwa na makosa mbalimbali katika utunzaji wa mazingira hayo kuwa ni pamoja na kutozwa faini isiyopungua shilingi elfu hamsini kwa makosa ya kutokuvaa sare na kutokupima afya zao wakiwa katika mazingira ya biashara zao.

Kwa upande wake katibu wa baraza la afya kata ya njombe mjini bwana Danda Ignas akiongea na mtandao huu kwa njia ya simu amesema kuwa, takribani watu kumi na tatu wameshikwa na kupewa adhabu ndani ya mwezi huu wa kumi na moja kwa makosa mbali mbali likiwemo kosa la kufanya biashara bila kupima afya na kutiririsha maji machafu ambapo kila mmoja ametozwa faini ya shilingi elfu ishirini badala ya elfu hamsini.

Monday, November 22, 2010

MBOLEA ZA RUZUKU MKOANI NJOMBE

MBOLEA ZA RUZUKU MKOANI NJOMBE ZAPUNGUZA MACHUNGU KWA
WANANCHI WILAYANI HUMO.


Wananchi wilayani Njombe Mkoani Iringa wamefurahishwa na kitendo cha utaratibu waserikali kubandika majina yao mapema juu ya watakao nufaika na mbolea za ruzuku ili kuondoa usumbufu wa kupanga foleni bila kujua kama watapata vocha.

Waandaaji wa safu hizi wamefanikiwa kufika katika Ofisi ya Serikali ya mtaa wa kibena kati na kuwakuta wananchi wakitazama majina yao.katika maoni yao wamevishukuru vyombo vya habari kwa kutangaza ubadhilifu uliotokea mwaka jana katika ugawaji pembejeo hizo na kudai kuwa vimepeleka kuweka utaratibu.

Aidha Afisa Mtendaji wa mtaa huo bwana OTMAR DANIEL MBANGALA ametoa maelekezo ya upokeaji vocha hizo kuwa ni lazima kujaza fomu ya mnufaika wa pembejeo hizo na kwamba yeyote ambaye hataridhika na mfumo huo anatkiwa kuwasilisha malalamiko yake kwenye balaza la kijiji.

Katika hatua nyingine amewataka wananchi hao kutoleta vurugu pindi vocha hizo zitakapo anza kutolewa kwani watakao simamia mchakato huo hawatanufaika na pembejeo hizo kwani watafanya kazi hiyo kwa kujitolea bila malipo hivyo amewataka kujua kuwa kwa mtaa huo wamepata vocha 1150 na kuwepo na upungufu wa vocha 1339.

Akijibu swali la wananchi waliouliza juu ya mabadiliko ya bei za pembejeo hizo kwa karibu kila mwaka,Bwana kindamba ambaye ni wakali wa pembejeo hizo katika mtaa wa kibena kati amewataka kujua kuwa mamlaka ya kubadili bei hizo ni mamlaka ya wahisani wenyewe wanaoleta pembejeo hizo.

Tuesday, November 16, 2010

TATIZO LA MAJI MKOA WA IRINGA

TATIZO LA MAJI MKOA WA IRINGA
KIJIJI CHA MIGOLI.


Wananchi wa Kijiji cha Migoli Mkoani Iringa wameelezea adha kubwa ya maji wanayoipata kwa kipindi cha miezi sita sasa kutokana na kuharibika kwa mtambo wa kusukumia maji kijijini hapo.

Wananchi hao Wamesema Awali walikuwa wakipata huduma hiyo ya maji kutoka kijiji cha Izazi kilichopo kilomita kumi kutoka Iringa lakini kwa kipindi cha miezi sita sasa tangu kuharibika kwa mtambo huo hali ya maisha imekuwa ngumu kwao kutoka na tatizo hilo la maji kwa maeneo mengi ya kijiji hicho.

Kutokana na hali hio imewalazimu wananchi hao kutumia maji kutoka Bwawa la Mtera na visima vya kuchimba kwa mkono ambapo imeelezwa kuwa maji wanayokuwa wanayapata kutoka katika vyanzo hivyo yametajwa kutokuwa Salama kwa matumizi ya Binadamu na kuwapelekea kuwasababishia magonjwa ya kuahara na kichocho miongoni mwao wakiwa watoto wadogo katika kijiji hicho.

Mhandisi wa Maji wa Wilaya ya Iringa Bw Lukas Madaha Amesema Tayari Idara yake imeanza hatua za Awali katika kulitatua Tatizo hilo linalowakabili wakazi hao wa kijiji hicho cha Migoli mkoani Iringa.

Friday, November 12, 2010

ATAKIWA KUFUATILIA MAUDHURIO YA WATOTO WAO.

WAZAZI WATAKIWA KUFUATILIA MAUDHURIO YA
WATOTO WAO WAKIWA SHULE.

.

Wazazi wilayani Njombe mkoani Iringa wametakiwa
kufuatilia mahudhurio ya watoto wao mashuleni ili kuweza
kujua maendeleo yao kiundani katika kuboresha kiwango cha elimu wilayani hapa.

Hayo yamebainishwa na mkaguzi mkuu wa shule za msingi wilayani Njombe BI.SARAH CHIWANGU ambaye amepewa dhamana ya kukagua shule mbalimbali katika kipindi hiki cha mitihani ya kidato cha pili akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake.,BI.CHIWANGU ameeleza kuwa halmashauri ya wilaya ya njombe ina jumla ya shule 53 zenye wanafunzi wa kidato cha pili wanaoendelea kufanya mtihani huo,ambapo halmashauri ya mji ina jumla ya shule 19,na halmashauri ya wilaya ina jumla ya shule 34 ambazo zinakamilisha idadi hiyo.

Aidha,ameyataja baadhi ya matatizo ambayo yamewapelekea baadhi ya wanafunzi kushindwa kufanya mitihani hiyo, kuwa ni pamoja na utoro ugonjwa na maradhi mbalimbali hali inayoweza kupelekea kushuka kwa kiwango cha taaluma wilayani hapa.

Katika hatua nyingine amewataka wanafunzi wa kidato cha kwanza ambao wanatarajia kufanya mtihani huo mwakani kujua umuhimu wa kufanya mitihani ya kidato cha pili kwani ndio inayowapa nafasi ya kuja kufanya mtihani wa kidato cha nne hivyo wasijisahau kwa vile hakuna mchujo wa kuingia kidato cha tatu.

Tuesday, November 9, 2010

WANANCHI WATAKIWA KULIPA KODI ZA MAJENGO YAO.NOMBE

WANANCHI WILAYANI NJOMBE MKOANI IRINGA WAMETAKIWA KULIPA KODI ZA MAJENGO YAO.

Wananchi Wilayani Njombe Mkoani Iringa wametakiwa kulipa kodi ya majengo ya nyumba zao kabla ya mabadiliko ya bei mpya itakayoanza mapema ifikapo Januari 2011kutokana uthaminishaji mpya wa majengo kutoka wizara ya ardhi.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa mtaa wa NAZARETH bwana COMRED JOHN .J.MTITU akizungumza na na mwandishi wa habari hii ofisini kwake juu ya mabadiliko ya bei mpya za kodi za ardhi.

Bwana MTITU amesema kuwa wananchi wa wamaeneo yake kama NAZARETH wanatakiwa kufika katika ofisi ya Melinze na wengine kufika kwenye shule mpya inayoendelea kujengwa Nazareth ilikupewa bei halisi ya nyumba ya kila mmoja ili kuepusha usumbufu unaoweza kujitokeza kutokana na mabadiliko hayo.

Akitolea mfano wa ongezeko la bei ya nyumba moja ya bwana TEUDOLI MLOWE mkazi wa NAZARETH, mwenyekiti huyo amesema,bei ambayo inafahamika ni shilingi Elfu tatu lakini bei mpya iliyofika kwenye nyumba ya bwana huyo mpaka sasa ni zaidi ya shilingi elfu ishirini na nne.

Aidha ameongeza kuwa,kwa wale wote walioomba kupimiwa viwanja vyao wanatakiwa kufika kulipia fedha kwaajiri ya zoezi hilo kwani MKURABITA wanaohusika na suala hilo watafanya kazi hiyo mpaka November 30 mwaka huu tu hivyo atakayepuuzia zoezi hilo hataweza kusaidiwa.

VYANDARUA KUGAIWA WILAYANI NJOMBE

KUTOKA KATIKA WILAYA YA NJOMBE.
VYANDARUA TUJIKINGE NA MALARIA.


Wananchi ambao hawakuandikishwa kupewa vyandarua Wilayani Njombe Mkoani Iringa wametakiwa kutolalamika pindi ugawaji vyandarua hivyo utakapo anza kwani idadi ya vyandarua vilivyofika ni vya walioandikishwa tu.

Rai hiyo imetolewa na Afisa mtendaji wa mtaa wa Melinze na Nazareth bwana EZEKIEL NJAWIKE akizungumza na Mwandishi wa Habari hii ofisini kwake juu ya ujio wa vyandarua hivyo katika mitaa yake.

Bwana NJAWIKE amesema kuwa Vyandarua alivyopewa katika maeneo yake,mtaa wa MELINZE amepewa jumla ya vyandarua 920 na mtaa wa NAZARETH amepewa jumla ya vyandarua 720 ambavyo ni idadi ya wananchi walioandikishwa,hivyo kwa wale waliohamia kipindi cha karibuni na wale ambao hawakuwepo wakati wa kuandikishwa ndio watakaokosa vyandarua hivyo.

Aidha ameongeza kuwa kwa mujibu wa ratiba ya wizara ya afya juu ya ugawaji vyandarua hivyo vitaanza kusambazwa ifikapo November 12 mpaka 14 kwa muda wa siku tatu na kukamilika kwa zoezi hilo hivyo watakaoshindwa kufika kwenye vituo hivyo kwa siku zote tatu hawata weza kupata vyandarua hivyo.

Katika hatua nyingine amewata wananchi hao kufuata maelekezo yaliyoandikwa kwenye kuponi juu ya vituo vya kwenda kuchukua vyandarua hivyo,kwani atakayekwenda tofauti na kituo alichoandikiwa hawezi kupata vyandarua hivyo na kwa mujibu wa muda wa kuanza kugawa ni kuanzia majira ya saa mbili asubuhi mpaka majira ya saa kumi kamili za jioni.

Monday, November 1, 2010

TUMEMALIZA UCHAGUZI SALAMA LAKINI HIVI NI VIJIMABO VILIVYOJILI..

BAADHI YA MAJIMBO HAWA WAGOMBEA KWELI WAMECHUANA..

MATOKEO ya awali ya kura za urais, ubunge na udiwani yaliyoanza kutolewa jana kwenye vituo mbalimbali nchini, yameonyesha kuwa nyota ya mgombea urais kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willibrod Slaa, imeendelea kung’ara huku wagombea ubunge wa chama hicho nao wakionekana kufanya vizuri.

Habari kutoka Jimbo la Iringa Mjini, zinasema matokeo ya urais katika kata saba, mgombea wa urais wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa, alikuwa akiongoza dhidi ya mgombea wa CCM, Jakaya Kikwete.

Vituo hivyo ni stendi, Dk. Slaa (146), Kikwete (114), Ndiuka Dk. Slaa (133), Kikwete (272), Soko Kuu 2, Dk. Slaa (114), Kikwete (84), Zimamoto 1, Dk. Slaa (93), Kikwete (84), Zimamoto 2, Dk. Slaa (84), Kikwete (108), Hazina Dk. Slaa (138), Kikwete (97), IDYC Dk. Slaa (75) na Kikwete (72).

Katika Jimbo la Mbeya Mjini, matokeo ya ubunge vituo vya Block T- A, CHADEMA (140), CCM (33), kituo B, CHADEMA (115) na CCM (15).

Mbeya Mjini, katika Kata ya Mwakibete, Dk. Slaa (3,564), Kikwete (950), Kalobe Sekondari 1 Dk. Slaa (109), Kikwete (97), Kalobe Sekondari 2 Dk. Slaa (107), Kikwete (76), Kalobe Sekondari 5 Dk. Slaa (93) na Kikwete (85).

Geita kura za urais Kikwete (376), Dk. Slaa (341), kwa upande wa ubunge CCM (396), CHADEMA (322) na CUF (10) na kwa udiwani CCM (315), CHADEMA (474) na CUF (0).

Jimbo la Kyela matokeo ya urais katika kituo cha Nsesi, Kikwete 150, Slaa 119, kituo cha Katumba shuleni Kikwete 150, Slaa 120, Kilasilo, Slaa 36, Kikwete 205, Community Centre Slaa 125, Kikwete 56, Itungi Slaa 76, Kikwete 54. Katika kituo cha Bunge, jijini Dar es Salaam, Slaa 225, Kikwete 189.Arusha Mjini, katika Kata ya Kaloleni A1, Dk. Slaa amepata kura (112), Kikwete (59), Kaloleni A2, Dk. Slaa (119), Kikwete (76), Profesa Lipumba (2), Kaloleni A3, Dk. Slaa (104), Kikwete (61), Lipumba (1), Kaloleni A4, Dk. Slaa (109) na Kikwete (165).

Kituo B1, Dk. Slaa (118), Kikwete (67), Profesa Lipumba (0), kituo B2, Dk. Slaa (102), Kikwete 64, B3, Slaa 92, Kikwete 50, B4, Slaa 87, Kikwete (67) na Lipumba (3).

Jimbo la Segerea, Kata ya Kipawa, kituo Minazi mirefu A1 urais, Kikwete (79), Dk. Slaa (75), Profesa Lipumba (7), kituo A6, Dk. Slaa (69), Kikwete (62), kituo A2, Dk. Slaa (102), Kikwete (52), Profesa Lipumba (1), kituo B3, Kikwete (64), Dk. Slaa (78) na Profesa Lipumba (3).

Katika matokeo ya ubunge wa kata hiyo, mgombea wa CHADEMA, Godbels Lema alionekana akiongoza ambapo katika Kata ya Kaloleni A1, (113), dhidi ya mgombea wa CCM, Dk. Batilda Burian (54), Kaloleni A2, Lema (120), Burian (71), Kaloleni A3, Lema (109), Batilda (62), Kaloleni A4, Lema (111) na Batilda (63).

Jimbo la Ukerewe katika vituo vitatu, Mtoni, Nansio, Bwisya, mgombea wa CHADEMA, Salvatory Namuyaga wa CHADEMA alikuwa akiongoza akifuatiwa na mgombea wa CCM, Gertrude Mongela.

Katika Jimbo la Musoma Mjini, CHADEMA ilikuwa ikiongoza kwa madiwani katika kata nane, CCM ikipata kata tatu na CUF ikipata madiwani wawili.

Taarifa za awali zimedokeza kuwa Vincent Nyerere, alikuwa akiongoza kwa tofauti kubwa dhidi ya mgombea wa CCM, Vedasto Manyinyi.

Jimbo la Moshi Mjini, CHADEMA ilikuwa ikiongoza kwa kiti cha urais na ubunge huku upande wa madiwani ilikuwa ikiongoza kwa kupata viti 15 kati ya 21.

Hali hiyo, ilijitokeza katika majimbo ya Kigoma Mjini na Kigoma Kaskazini, ambako upinzani mkubwa ulikuwa kati ya vyama vya CCM na CHADEMA.

Katika Jimbo la Kigoma Mjini, Peter Serukamba wa CCM anachuana na Ally Mleh wa CHADEMA, huku katika Jimbo la Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe wa CHADEMA anachuana na Robinson Lembo wa CCM.

Jimbo la Mbeya Mjini, mpaka tunakwenda mitamboni mgombea wa CHADEMA, Joseph Mbilinyi, ameonekana kuongoza dhidi ya mgombea wa CCM, Benson Mpesya.

Kituo Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam (DARUSO), urais Dk. Slaa (454), Kikwete (71), ubunge, John Mnyika wa CHADEMA (473) na Hawa Ng’umbi wa CCM (45).

Maswa, Magharibi, ubunge

Mgombea wa CHADEMA, John Shibuda, alikuwa akiongoza dhidi ya mgombea wa CCM, Peter Kisena, ambapo katika kituo cha Bukigi, Kata ya Malampaka Shibuda 113, Kisena 65, Sokoni Shibuda 68, Kisena 46, Sokoni B Shibuda, 61, Kisena 56, Mahakama A, Shibuda 66, Kisena 47, Mahakamani B, Shibuda 65, Kisena 50.

Shule ya Msingi Malampaka, Shibuda 54, Kisena 55, Chekechea A Shibuda 79 Kisena 5, Chekechea B, Shibuda 74, Kisena 53, Oil Mill, Shibuda 56, Kisena 36.

Jimbo la Nyamagana, inadaiwa mgombea wa ubunge Ezekiel Wenje, ameonekana kuongoza dhidi ya mgombea wa CCM, Lawrence Masha, ambaye ni Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi.

Katika jimbo hilo CHADEMA inaongoza kwa kupata madiwani katika kata 12 kati ya 14.

Katika Jimbo la Iringa Mjini, hadi tunakwenda mitamboni mgombea wa CHADEMA, Peter Msigwa, alikuwa akiongoza katika vituo vingi dhidi ya mgombea wa CCM, Monica Mbega.



DAR ES SALAAM NA MBEYA NAKO HALI ILIKUWA NI TETE
MASANDUKUKU TENA.?




ZOEZI la upigaji kura nchini limefanyika jana, huku zikiripotiwa kasoro kadhaa na baadhi ya watu wakikamatwa na kura za wizi pamoja na polisi kulazimika kupiga mabomu ya machozi.

Mjini Dar es Salaam, eneo la Mwananyamala Kisiwani, jana liligeuka uwanja wa vita, baada ya askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), kulazimika kupiga mabomu ya machozi kwa ajili ya kutawanya mamia ya wananchi waliokuwa karibu na eneo hilo.

Tuki hilo lilitokea majira ya saa 8:40 mchana baada ya wananchi kutilia shaka moja ya gari la waangalizi lililofika eneo hilo, wakidai lina boksi la kura zilizopigwa.

Tukio hilo, lilionekana kutaka kuvunja amani, hali iliyosababisha askari kupiga mabomu kwa lengo la kutawanya mamia ya wananchi walioonekana wakiwa wamejawa na hasira.

Baada ya kuona hali inazidi kuwa mbaya, mmoja wa maofisa waliokuwepo eneo hilo, alilazimika kuomba msaada wa askari zaidi ambao walifika wakiwa kwenye magari ya PT 2061, PT 0886 na PT 1523, likiwamo gari la kurusha maji ya kuwasha.

Kuwasili kwa magari hayo kulionekana wazi kupunguza kasi ya wananchi ambao awali walirusha mawe bila kujali kitu chochote kilichokuwa mbele yao.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni, Elias Kalinga, aliyefika eneo hilo aliwaambia waandishi wa habari kuwa mbali na tukio hilo, hali ilikuwa shwari karibu katika vituo vyote.

“Ni kweli hapa kumetokea tukio hili, lakini kama mnavyoona hali imetulia, wananchi na kazi zinaendelea kama kawaida... maeneo yote yako shwari jamani kama mlivyoona,” alisema Kamanda Kalinga.

Katika tukio mbalo linaonekana kushtua watu wengi, ni pale mwanamke mmoja alikamatwa akiwa na mfuko wa rambo uliojaa kura zinazodaiwa kupigiwa mgombea mmoja wa urais huku akiwa kibindoni na sh 600,000.

Mwanamke huyo ambaye aligoma kutaja jina lake, alikamatwa na kupelekwa kituo cha polisi Minazini kabla ya kuchukuliwa na kuhamishiwa Kituo cha Polisi Oysterbay.

Kamanda Kalinga alipoulizwa na waandishi wa habari alikiri kuwepo kwa tukio hilo na kuahidi kulitolea ufafanuzi leo baada ya uchunguzi kukamilika.

Katika tukio jingine, ni pale lilipowasili gari la Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), aina ya IVECO lenye namba za usajili 9003 JW 09 katika eneo hilo, hali iliyosababisha wananchi wengi kupigwa butwaa.

Lakini katika maeneo ya Kawe, Manzese, Sinza, Kigogo, Buguruni, TAZARA, Kinondoni, Msasani, Bunju, Ukonga, Kimara hadi jana jioni hali ilikuwa ni shwari.

Moja ya malalamiko makubwa katika maeneo mengi lilikuwa ni ukosefu wa majina mengi ya wapiga kura licha ya kuwa na shahada.

Mkoani Mbeya, kabla zoezi la kupiga kura, kulibainika kuwepo kwa njama za wizi wa kura baada ya kukamatwa kwa masanduku ya kupigia kura yakiwa na karatasi za kupigia kura kwa nafasi ya ubunge na urais.

Masanduku hayo yalikutwa juzi usiku nyumbani kwa msimamizi wa kituo cha Makole ambaye ni mwalimu, Wabuga Tarimo ambaye alitakiwa kuwa kituoni kwake kwenye kata hiyo, lakini alikiuka sheria na maagizo ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) na kuondoka na masanduku hayo yakiwa na karatasi za kupigia kura.

Baada ya wapiga kura kubaini njama hizo, huku wakidai wana haki ya kufahamu chimbuko la tukio hilo, wamelazimika kuweka ulinzi katika nyumba hiyo na kutoa taarifa kituo cha polisi ili kukamata vifaa hivyo.

Ofisa Upelelezi wa Makosa ya Jinai wa Wilaya ya Dodoma, Jonathan Shani, alifika eneo la tukio na kuendesha upekuzi, alibaini uwepo wa masanduku hayo ambayo yalikuwa na karatasi za kupigia kura ambazo zilikuwa za wagombea ubunge na urais.

Kamanda huyo akiwa na mashuhuda walifungua masanduku na kubaini kuwa kura hizo bado hazijawekewa tiki.

Tukio hilo, liliwashutua wapiga kura wengi ambao walieleza hali hiyo inadhihirisha wazi kuwa ni dalili tosha za kufanya njama za kuiba kura, jambo ambalo linaweza kuathiri matokeo ya kweli.

Baada ya kufanikiwa kuyakamata masanduku yao ambayo yalikuwa nyumbani kwa msimamizi huyo, kinyume cha utaratibu alipelekwa moja kwa moja kituo cha polisi ili kuhojiwa kwa lengo la kutaka kujua sababu za kuweka vifaa hivyo nyumbani kwake.

Akiwa chini ya ulinzi uliokuwa ukiongozwa na Ofisa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Wilaya ya Dodoma Mjini, mtuhumiwa huyo, alidai alilazimika kwenda na vifaa hivyo nyumbani kwake kwa kuwa kituo cha kupigia kura kilikuwa mbali na hakuwa na ulinzi wowote.

Pamoja na tukio hilo kushuhudiwa na Kamanda wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Dodoma Zelote Stephen, alipohojiwa kuhusu suala hilo alisema hajapata taarifa zozote.

KONDOA NAKO

Vibanda vya kupigia kura katika Wilaya ya Kondoa vimechomwa moto na watu wasiojulikana na kusababisha wasimaamizi na wapiga kura kuendesha shughuli zao katika mazingira ya jua kali.

Tukio hilo lilithibitishwa na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Dodoma, Zelote Stephen, na kudai kuwa vibanda hivyo viliunguzwa na watu wasiojulikana, japo hakuna hasara yoyote iliyotokea.

NAKO KAWE

Mgombea ubunge wa Jimbo la Kawe kwa tiketi ya Chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia na baadhi ya wananchi, wameshindwa kupiga kura baada ya majina yao kukosekana katika vituo walivyojiandikishia.

Hali hiyo ilijitokeza jana majira ya saa 2 asubuhi, baada ya mgombea huyo kufika katika kituo namba tatu cha Sokoni Juu, kwa ajili ya kupiga kura, lakini jina lake lilikosekana katika daftari la wapiga kura.

Akizungumzia kitendo hicho, Mbatia alisema watu wengi watapoteza haki zao kutokana na kushindwa kupata majina yao.

“Wakati wa zoezi la kuhakiki majina nilifika ili kuangalia jina langu…nilipolikosa nilifanya mawasiliano ili kujua lililojitokeza huku nikiwa na shahada yangu namba 17460120 lakini NEC ilidai kulijishughulikia suala hilo,” alisema Mbatia.

HUKO KASURU VIJIJINI NAKO.

Wananachi wa kata za Nyachenda na Kitagata, zilizopo Jimbo la Kasulu Vijijini, wameshindwa kupiga kura za udiwani kutokana na kutokuwapo kwa karatasi za kupigia kura na kifo cha mgombea.

Mratibu wa uchaguzi mkoani Kigoma, Anthony Jakonyango, alisema katika Kata ya Kitagata uchaguzi haukuweza kufanyika kutokana na kutokuwepo kwa karatasi za kupigia kura.

Wakati Kata ya Nyachenda uchaguzi haukuweza kufanyika kutokana na kifo cha mgombea udiwani wa kata hiyo, kwa tiketi ya Chama cha NCCR-Mageuzi, Bernard Machupa, aliyefariki dunia wiki tatu zilizopita.

Alisema mpaka sasa haijafahamika wananchi hao watapiga lini kura, kwani tume bado haijapanga tarehe ya uchaguzi.

Mbali na kasoro hizo, uchaguzi mkoani Kigoma umefanyika kwa amani na watu walianza kujitokeza vituoni tangu saa 12:30 asubuhi kabla ya muda wa kufungua vituo.

Katika Jimbo la Kigoma Mjini, Peter Serukamba wa CCM anachuana na Ally Mleh (CHADEMA), huku katika Jimbo la Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe wa CHADEMA anachuana na Robinson Lembo wa CCM.

HUKO MBEYA MJINI

Hali ilikuwa tete katika kituo cha Mzalendo, jimboni hapa, baada ya wananchi kutishia kutopiga kura kutokana na wasimamizi wa kituo hicho kuingia kwenye chumba cha kupigia kura wakiwa na makoti makubwa na mabegi, hali iliyowapa wasiwasi wapiga kura.

Kutokana na hali hiyo, wananchi waliwataka wasimamizi kuvua makoti waliyovaa pamoja na mabeki na kuwataka wayatoe nje kabla ya zoezi la upigaji kura kuanza, jambo ambalo wasimamizi hao walilitii na kuruhusu upigaji kura kuendelea.

Hata hivyo, wananchi hao walieleza kasoro nyingine katika kituo hicho kuwa ni kutokuwepo kwa askari wa kusimamia kituo, hali ambayo iliwatia wasiwasi endapo kungetokea vurugu.


HUKO ARUSHA

Mgombea ubunge wa Jimbo la Arusha kwa tiketi ya CHADEMA, Godbles Lema, amejeruhiwa kwa jiwe katika mguu wake wa kushoto na kada wa CCM anayefahamika kwa jina la Musa Abdallah, ambaye hivi sasa anashikiliwa na polisi.

Mbali na tukio hilo, daftari la wapiga kura katika Kata ya Sombetini lenye majina 470 limeibwa jana majira ya saa 3:30 asubuhi katika mazingira ya kutatanisha.

Kutokana na matukio hayo, msimamizi wa kituo hicho, Charles Munis, anashikiliwa na polisi. Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha, Basilio Matei, amethibitisha kutokea kwa matukio hayo.

Taarifa hii imeandaliwa na Danson Kaijage (Dodoma), Iddi Risasi (Kigoma), Christopher Nyenyembe na Mosses Ng’wat (Mbeya), Grace Macha (Moshi), Ramadhani Siwayombe (Arusha), Neema Kishebuka (Tanga) na Betty Kangonga (Dar).



TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imetangaza kuahirisha uchaguzi katika majimbo matatu na kata 23 kutokana na upungufu wa karatasi za kupigia kura.

Mkurugenzi wa NEC, Rajab Kiravu aliyataja majimbo hayo jana kuwa ni Nkenge, Mpanda Mjini na Mpanda Vijijini.

Alisema katika majimbo hayo matatu ambayo uchaguzi umeahirishwa wapiga kura wataendelea kupiga kura ya rais na madiwani kama ulivyopangwa.

Aidha, alizitaja kata ambazo zimesimamishwa uchaguzi wake ni Endegikot iliyopo Mbulu, Mbede iliyopo Mpanda, Kisiwani iliyopo Same na Kata ya Matonya iliyopo Newala.

Kata nyingine ni Mji Mwema iliyopo Njombe, Kigwa na Ibelamikundi zilizopo Uyui, Kata za Gongo la Mboto iliyopo Ilala, Msogezi iliyopo Ulanga, Kimuli na Kamuli zilizopo Karagwe.

Kata za Kisanga iliyopo Sikonge, Mkuyuni na Mirongo za Mwanza, Kitagata iliyopo Kasulu, Buseresere iliyopo Chato na Mazinga iliyopo Muleba.

Mkurugenzi huyo alisema kata nyingine ni Kilangalanga iliyopo Kibaha na Kibiti, Chemchem, Ngorongo, Kipungira na Mjawa zilizopo Rufiji.

“Katika Kata ambazo uchaguzi wa madiwani umehairishwa uchaguzi wa rais na wabunge utaendelea kufanyika kama ulivyopangwa awali,” alisema Kiravu.

Alisema tume itatangaza baadye siku za kufanyika kwa chaguzi hizo zilizoahirishwa.

Akizungumza na Tanzania Daima jana, mgombea ubunge wa Mpanda Kati kwa tiketi ya chadema, Said Arfi, alisema hadi majira ya saa nane mchana jana hakuwa na barua rasmi ya kusimamishwa kwa uchaguzi huo.

Hata hivyo, alisema alishangaa asubuhi kusikia redioni na kwamba hakuwa na taarifa zozote za kutofanyika kwa uchaguzi jimboni hapo.