Saturday, September 12, 2015

Dr WILBROAD SLAA AWAPIGA JIWE LINGINE CHADEMA




ALIYEKUWA Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk Wilbrod Slaa amejitokeza hadharani kwa mara nyingine na kujibu watu waliojitokeza kuponda hotuba yake, aliyoitoa hivi karibuni kuwa hawana hoja zaidi ya kumtukana.

Akizungumza kupitia kituo kimoja cha Televisheni jijini Dar es Salaam, Dk Slaa alisema madai yote, yaliyotolewa juu yake na baadhi ya watu wakiwemo viongozi wa Chadema na vyama vinavyounda Ukawa, baada ya hotuba aliyoitoa, hayana msingi wowote na kwamba ni kuishiwa hoja, ndio maana walimtukana badala ya kujibu hoja.

“Nashukuru hoja zangu zote hawajazijibu, sasa wanapiga tu propaganda, hata Rostam Aziz alijaribu kujibu, lakini akatukana tu kama alivyonitukana mwaka 2007 badala ya kujibu hoja na mimi nasema ufisadi ni hoja,” alisema Slaa.

Aidha, Dk Slaa alisema hawezi kumpeleka mahakamani Rostam ambaye ni kada wa CCM, ambaye amemtaka Dk Slaa ampeleke mahakamani kama anao ushahidi kuwa anaunga mkono mgombea urais kwa tiketi ya Chadema, Edward Lowassa.

Slaa amesema yuko tayari kutoa ushahidi wake pale Jamhuri itakapomfungulia mashitaka. “Wale ambao hawaelewi taratibu za kesi, kuna kesi za madai ambapo mtu binafsi anafungua kesi na kesi za jinai ambazo mtu binafsi hawezi kufungua ila Jamhuri, kesi za Jamhuri mtu huwezi kufungua, wewe ni shahidi… mimi nikiitwa nitakwenda kutoa ushahidi dhidi ya Rostam Aziz,” alisema Dk Slaa.

Aidha, alisema ni kweli vijana wanataka mabadiliko na ni hoja ya msingi na pia wakulima ambao hawafaidiki na kilimo chao, wanataka mabadiliko, vivyo hivyo kwa makundi mengine.
 
 “Nimesema mimi Lowassa hafai, leo, lini ameanza kuwa rafiki wa masikini?

"Lini ameanza kuwa safi?Watanzania waache ushabiki usiofaa wapime kwa vigezo, ushabiki usio na tija utatuangamiza,” alisema Dk Slaa, akijibu hoja mbalimbali ambazo zimejitokeza baada ya hotuba yake hiyo, aliyoitoa mwanzoni mwa wiki hii baada ya kutangaza kuachana na mambo ya siasa na kubaki mshauri wa wananchi.

Akijibu shutuma dhidi yake baada ya kutuhumiwa kutoa habari za upotoshaji juu ya maaskofu, Slaa alisema alichokieleza siku ile anatangaza kujiengua kwenye siasa ni alichoambiwa na Mchungaji wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima kwamba maaskofu 30 kati ya 34 walihongwa.

“Tatizo halikuwa fedha bali askofu anaona sifa mimi kumuunga mkono mtu ambaye alitumia fedha kununua maaskofu, na Watanzania nawaomba mtulie msikurupuke na maneno bila kuyachambua, taifa linaangamia kwa sababu ya ushabiki usio na tija, nimeshtushwa na kauli yake, kiongozi anayepaswa kukemea rushwa, maovu… baba askofu piga magoti Mungu wako atazame dhamira yako,” alisema.

Dk Slaa alisema yeye ana uwezo wa kupambanua siasa na mambo mengine na kwamba ni kweli alikutana na Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe katika Hoteli ya Serena na hiyo ni katika kupata taarifa alizozihitaji kwa ajili ya kazi yake ya utafiti na kwamba Mwakyembe ni chanzo cha taarifa cha kwanza na kwamba hakufanya kwa siri.

Akizungumzia picha yake ambayo ilizunguka kwenye mitandao ya kijamii, ikimuonesha yeye akiwa na Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba na Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba alisema picha hiyo ni wakati wa mkutano wa vyama vya siasa na Rais wa Ujerumani, Joachim Gauck alipokuja kwenye ziara ya kikazi Februari mwaka huu.

“Kwenye picha hizo ambazo zinatuonesha mimi, Mwigulu na Profesa Lipumba tukimpokea Rais wa Ujerumani alipotembelea Tanzania, leo ndio zinaletwa kuonesha eti haya ndiyo mazungumzo ya kumng’oa Slaa, naomba niwaambie warudi nyuma waangalie hizo picha ni za lini hazina uhusiano na mimi kujiondoa,” alisema Dk Slaa.

Aidha, Dk Slaa alisema kuwa kuna propaganda nyingine ambayo imetumika ambapo watu wametuma pia picha ambazo zinamuonesha akiwa kwenye ndege, ikisemekana kwamba ametoroka nchini baada ya hotuba, sio kweli.

Alikiri kusafiri lakini sio kwa kutoroka, kama ambavyo imedaiwa na baadhi ya watu na kwamba amekuwa akipiga picha na watu kwenye ndege na kwamba picha hiyo ni ya safari ambayo alishasafiri na kurudi.

“Magazeti na mitandao wanasema Dk Slaa hayuko nchini, lakini nadhani sasa Watanzania wanaona sasa niko hapa studio Dar es Salaam na siko Marekani,” alisema Dk Slaa na kuongeza kuwa uongo huo unaonesha ni aina gani za siasa zilizopo hapa nchini.


Alisema hoja ya wapi amepata fedha kwenda Serengeti na kuishi hotelini ni hafifu. “Nilikwenda Marekani na kukaa kwa zaidi ya miezi 12 na kutembelea majimbo 13 na sikulipiwa na mtu yoyote zaidi ya chama changu kulipia shilingi 500,000 kwa mshauri aliyeandaa nyaraka ya kunisaidia katika ziara hiyo, mbona hawakuniuliza nimepata wapi fedha hizo?”

wafuasi wa chama cha demokrasia na maendeleo chadema na chama cha mapinduzi ccm wapigana na kusababisha mauaji




Wanachama na wafuasi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), juzi walishambuliana kwa ngumi na silaha za jadi na kusababisha kifo cha mtu mmoja na kujeruhi wengine watano.

Tukio hilo limetokea saa 4.09 asubuhi katika Kijiji cha Mangucha, Wilaya ya Tarime mkoani Mara wakati wanachama na wafuasi wa vyama hivyo wakiwa kwenye shughuli za kampeni za vyama vyao. 

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi wa Tarime na Rorya, Lazaro Mambosasa, alisema chanzo cha vurugu hizo ni mapambano yaliyohusisha silaha za jadi baada ya wafuasi wa Chadema kufanya maandamano ya kwenda kuwapokea wagombea ubunge na udiwani waliokuwa wakitokea Kijiji cha Mwambara kwenda Kijiji cha Kegonga ambako pia kulikuwa na mkutano wa kampeni za CCM.

Kamanda Mambosasa alisema wafuasi wa Chadema walipofika eneo ambalo wana CCM walikuwa wakifanya mkutano wao walinyoosha mikono juu huku wakionyesha alama ya vidole viwili ambayo huitumia kwa salamu kitendo ambacho kiliamsha hasira za wafuasi wa CCM na ndipo mapambano hayo yalipotokea.

Alimtaja aliyeuawa katika mapambano hayo kuwa ni Mwita Bhoke Waite (37) ambaye ni mkazi wa Kijiji cha Nyandage baada ya kushambuliwa na kitu chenye ncha kali kifuani na kwenye paja la mguu wa kushoto.

Kamanda Mambosasa aliwataja waliojeruhiwa kuwa ni Chacha Mwita Chacha (32) mkazi wa Kijiji cha Nyasage ambaye alijeruhiwa mgongoni, mguuni na mkononi, Kimunye Chacha Mgesi (54) mkazi wa Kegonga aliyejeruhiwa mikono yote miwili na kichwani pamoja na Elizabeth Wiliam Marwa (43) ambaye ni mtumishi wa CCM Wilaya ya Tarime alijeruhiwa sehemu mbalimbali za mwili kwa kupigwa na ubapa wa panga.

Majeruhi wengine aliowataja ni Oueen Ryoba (47) ambaye ni mfanyabiashara aliyejeruhiwa sehemu mbalimbali za mwili kwa kupigwa na ubapa wa panga na Nyaitati Marianya (30), mkazi wa Kegonga aliyejeruhiwa mkononi.

Akizungumzia mwenendo wa uchunguzi wa tukio hilo, Kamanda Mambosasa alisema Jeshi la Polisi linawashikilia watu wanne wanaotuhumiwa kuwa chanzo cha vurugu hizo.

Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Kius Matiko (28) mkazi wa Kijiji cha Kegonga, Nyambari Nchagwa (43) mkazi wa Kijiji cha Nyandage, Marwa Samweli (25) na Magasi Samweli Ghati, wote wakazi wa Kijiji cha Kegonga Wilaya ya Tarime.

Naye Muuguzi Mfawidhi wa Hospitali ya Tarime, Rose Hosea, alipoulizwa kuhusu hali za majeruhi waliofikishwa hospitalini hapo alisema wanne wanaendelea vizuri na matibabu isipokuwa mmoja aliyemtaja kwa jina la  Chacha Mwita Chacha ambaye  amehamishiwa Hospitali ya Musoma kwa matibabu zaidi kutokana na majeraha makubwa aliyoyapata.

Wakati huo huo, taarifa zilizolifikia gazeti hili wakati linakwenda mitamboni zimeeleza kuwa gari la mgombea ubunge wa Jimbo la Tarime Mjini, Esther Matiko limeharibiwa vibaya katika mapambano hayo.


Alisema gari hilo lenye namba za usajili T 282 DEE lilishambuliwa kwa mawe wakati wa mapambano hayo yakiendelea na imekuwa vigumu kutambua mara moja waliohusika na uharibifu huo.