Thursday, September 28, 2017

UVCCM YAFANYA UCHAGUZI KUWAPATA VIONGOZI WAPYA WILAYANI KILOSA

Umoja wa vijana wa chama cha Mapinduzi UVCCM Wilaya ya Kilosa Septemba 25 mwaka huu wamefanya uchaguzi wa Viongozi wa ngazi mbalimbali akiwemo Mwenyekiti wa Vijana kwa mujibu wa katiba ya chama hicho.
Uchaguzi huo umefanyika kwenye ukumbi wa MT lodge uliopo Mjini Kilosa na kuudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa chama hicho wa Wilaya na ambapo ndugu Salehe  Nasibu Mhando amefanikiwa kuchaguliwa kuwa mwenyekiti wa umoja wa vijana Wilaya kwa kupata ushindi wa jumla ya kura 311 na kuwapita wapinzani wenzake wawili ambao ni Malko Madenge aliepata kura 65, Catherine Mtugo aliepata kura 134 ambapo idadi ya kura zote zilizopigwa ikiwa ni 524 huku zilizoharibika ni kura 14.

Akizungumza baada ya kuapishwa mwenyekiti huyo mpya Salehe Nasibu Mhando amesema anawashukuru wajumbe wote waliojitokeza kumpigia kura na kuahidi kuwa atahakikisha kutenga ofisi za Vijana katika kila eneo kuutumikia umoja wa Vijana wa chama cha mapinduzi kwa kutumia baraza la wilaya kwa kushirikiana na kamati ya utekelezaji ili kusaidia umoja huo kuwa na idadi kubwa ya vijana kwenye chama tawala.

Naye Mwenyekiti aliemaliza muda wake Michael Mkolokoti amemshauri Mwenyekiti Huyo mpya kuhakikisha anawasaidia vijana kwa kuwaondoa katika hali ya kutumika vibaya bila manufaa hasa kipindi cha uchaguzi.