Saturday, September 12, 2015

wafuasi wa chama cha demokrasia na maendeleo chadema na chama cha mapinduzi ccm wapigana na kusababisha mauaji




Wanachama na wafuasi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), juzi walishambuliana kwa ngumi na silaha za jadi na kusababisha kifo cha mtu mmoja na kujeruhi wengine watano.

Tukio hilo limetokea saa 4.09 asubuhi katika Kijiji cha Mangucha, Wilaya ya Tarime mkoani Mara wakati wanachama na wafuasi wa vyama hivyo wakiwa kwenye shughuli za kampeni za vyama vyao. 

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi wa Tarime na Rorya, Lazaro Mambosasa, alisema chanzo cha vurugu hizo ni mapambano yaliyohusisha silaha za jadi baada ya wafuasi wa Chadema kufanya maandamano ya kwenda kuwapokea wagombea ubunge na udiwani waliokuwa wakitokea Kijiji cha Mwambara kwenda Kijiji cha Kegonga ambako pia kulikuwa na mkutano wa kampeni za CCM.

Kamanda Mambosasa alisema wafuasi wa Chadema walipofika eneo ambalo wana CCM walikuwa wakifanya mkutano wao walinyoosha mikono juu huku wakionyesha alama ya vidole viwili ambayo huitumia kwa salamu kitendo ambacho kiliamsha hasira za wafuasi wa CCM na ndipo mapambano hayo yalipotokea.

Alimtaja aliyeuawa katika mapambano hayo kuwa ni Mwita Bhoke Waite (37) ambaye ni mkazi wa Kijiji cha Nyandage baada ya kushambuliwa na kitu chenye ncha kali kifuani na kwenye paja la mguu wa kushoto.

Kamanda Mambosasa aliwataja waliojeruhiwa kuwa ni Chacha Mwita Chacha (32) mkazi wa Kijiji cha Nyasage ambaye alijeruhiwa mgongoni, mguuni na mkononi, Kimunye Chacha Mgesi (54) mkazi wa Kegonga aliyejeruhiwa mikono yote miwili na kichwani pamoja na Elizabeth Wiliam Marwa (43) ambaye ni mtumishi wa CCM Wilaya ya Tarime alijeruhiwa sehemu mbalimbali za mwili kwa kupigwa na ubapa wa panga.

Majeruhi wengine aliowataja ni Oueen Ryoba (47) ambaye ni mfanyabiashara aliyejeruhiwa sehemu mbalimbali za mwili kwa kupigwa na ubapa wa panga na Nyaitati Marianya (30), mkazi wa Kegonga aliyejeruhiwa mkononi.

Akizungumzia mwenendo wa uchunguzi wa tukio hilo, Kamanda Mambosasa alisema Jeshi la Polisi linawashikilia watu wanne wanaotuhumiwa kuwa chanzo cha vurugu hizo.

Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Kius Matiko (28) mkazi wa Kijiji cha Kegonga, Nyambari Nchagwa (43) mkazi wa Kijiji cha Nyandage, Marwa Samweli (25) na Magasi Samweli Ghati, wote wakazi wa Kijiji cha Kegonga Wilaya ya Tarime.

Naye Muuguzi Mfawidhi wa Hospitali ya Tarime, Rose Hosea, alipoulizwa kuhusu hali za majeruhi waliofikishwa hospitalini hapo alisema wanne wanaendelea vizuri na matibabu isipokuwa mmoja aliyemtaja kwa jina la  Chacha Mwita Chacha ambaye  amehamishiwa Hospitali ya Musoma kwa matibabu zaidi kutokana na majeraha makubwa aliyoyapata.

Wakati huo huo, taarifa zilizolifikia gazeti hili wakati linakwenda mitamboni zimeeleza kuwa gari la mgombea ubunge wa Jimbo la Tarime Mjini, Esther Matiko limeharibiwa vibaya katika mapambano hayo.


Alisema gari hilo lenye namba za usajili T 282 DEE lilishambuliwa kwa mawe wakati wa mapambano hayo yakiendelea na imekuwa vigumu kutambua mara moja waliohusika na uharibifu huo.

No comments:

Post a Comment