Wednesday, November 24, 2010

WATAKIWA KUPIMA AFYA ZAO NJOMBE MKOANI IRINGA

WAHUDUMU WA NYUMBA ZA KULALA WAGENI NA WAHUDUMU
MBALI MBALI WATAKIWA KUPIMA AFYA ZAO.


Wahudumu wa nyumba za kulala wageni (GUEST HOUSE) na wahudumu wa saloon za kike na za kiume wilayani Njombe Mkoani Iringa wametakiwa kujitokeza kupima afya zao badala ya kusubiri kukamatwa na maafisa wa afya.

Hayo yamebainishwa na Afisa afya wa halmashauri ya mji wa Njombe BI.Saada Milanzi akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake juu ya umuhimu wa utunzaji wa mazingira.

Akisoma kifungu cha sheria ya afya cha mwaka 2009 Bi.Milanzi amesema kuwa kifungu hicho kinawataka wafanyabiashara wote wa vyakula,wahudumu wa saloon na wahudumu wa nyumba za kulala wageni wanatakiwa kupima afya zao kila baada ya miezi sita lakini matokeo yake wahusika hao wamekuwa wakikaidi sheria hiyo.

Akieleza baadhi ya changamoto wanazokumbana nazo katika utendaji wa kazi amesema kuwa hospitali na zahanati za halmashauri ya mji wa Njombe zinakabiliwa na upungufu wa maafisa wa afya hali inayopelekea kushindwa kuwafikia wananchi wote kuwapa elimu juu ya utunzaji wa mazingira.

Katika hatua nyingine amezitaja baadhi ya adhabu ambazo zimekuwa zikitolewa n kwa wanaoshikwa na makosa mbalimbali katika utunzaji wa mazingira hayo kuwa ni pamoja na kutozwa faini isiyopungua shilingi elfu hamsini kwa makosa ya kutokuvaa sare na kutokupima afya zao wakiwa katika mazingira ya biashara zao.

Kwa upande wake katibu wa baraza la afya kata ya njombe mjini bwana Danda Ignas akiongea na mtandao huu kwa njia ya simu amesema kuwa, takribani watu kumi na tatu wameshikwa na kupewa adhabu ndani ya mwezi huu wa kumi na moja kwa makosa mbali mbali likiwemo kosa la kufanya biashara bila kupima afya na kutiririsha maji machafu ambapo kila mmoja ametozwa faini ya shilingi elfu ishirini badala ya elfu hamsini.

No comments:

Post a Comment