Wednesday, July 2, 2014

WAKAZI WA WILAYANI KILOSA MKOANI MOROGORO WATAKIWA KUJIANDAA NA ZOEZI LA USAJILI NA UTAMBUZI KWENYE DAFTARI LA WAKAZI



Wakazi wa Wilaya ya Kilosa Mkoani Morogoro wametakiwa kujiandaa na zoezi la usajili na utambuzi kwenye daftari la wakazi katika maeneo yao wanayoishi ili kupata kitambulisho cha Taifa ambacho ni muhimu kwa kila Mtanzania aliyefikisha umri wa kuanzia miaka 18 na kuendelea.
Wito huo umetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Elias Tarimo ofisini kwake wakati akizungumza kwenye kikao maalum kilichowahusisha Wakuu wote wa Idara na Viongozi mbalimbali Julai mosi mwaka huu.
Tarimo amesema kuwa zoezi la kujisajili na utambuzi kwa wananchi Mkoani Morogoro litazinduliwa rasmi na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Joel Bendera Agosti 4 mwaka huu lengo likiwa kila mwananchi ambaye ni Mtanzania halali aweze kupata kitambulisho cha Taifa.
Hatahivyo amesema kuwa ni jukumu la Maafisa watendaji wote kuhakikisha wananchi wamejiandikisha katika maeneo yao kwenye daftari la mkazi ili kurahisisha zoezi hilo litakapoanza pia amewataka kuacha kudai malipo yoyote kwani kazi hiyo ni wajibu wao.
Aidha Tarimo ameongeza kwa kusema kuwa hakuna mwananchi atakayepata Kitambulisho cha Taifa mpaka ajiandikishe kwenye daftari la mkazi katika eneo husika hivyo ni vyema kila mwananchi akajiandaa kuwa na vielelezo vya utambuzi kama vile kopi ya kitambulisho cha mpiga kura,cheti cha kuzaliwa,ubatizo, cheti cha ndoa,pasi ya kusafiria na vielelezo vingine ili iwe rahisi kutambulika pindi zoezi litakapoanza.
Zoezi la usajili na utambuzi kwa ajili ya vitambulisho vya Taifa linaendeshwa na serikali kupitia mamlaka ya vitambulisho vya Taifa (NIDA) ambapo Kitaifa limeanzia Mkoani Dar es salaam na kwa Mkoa wa Morogoro litazinduliwa rasmi mapema mwezi ujao mwaka huu.

No comments:

Post a Comment