Wednesday, July 9, 2014

WAKULIMA WILAYANI KILOSA WANUFAIKA NA MKUHUMI


Afisa Elimu kutoka shirika la mkuhumi Wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro Shadrack Yoash amewataka wakulima kuacha kulima kilimo cha mazoea na kinachoathiriwa na mabadiliko ya tabia ya nchi na badala yake walime kilimo cha kisasa ili waweze kuepukana na umasikini.
Hayo ameyasema julai 8 mwaka huu kwenye sherehe za wakulima wa shamba darasa zilizofanyika katika kijiji cha Lunezi kitongoji cha Manyomvi kata ya Lumuma Wilayani humo ambazo zimeandaliwa na Shirika lisilo la kiserikali Mkuhumi.
Yoash amesema kuwa mabadiliko ya tabia ya nchi yalivyo na kasi kwa kipindi hiki huku wananchi wakiendelea kulima kilimo cha mazoea hawataweza kupata mavuno ya kutosha na kwamba watazidi kukata misitu kwa ajili ya kuongeza mashamba hali itakayo sababisha kutokea kwa ukame na hatimaye wakulima kuwa na kipato kidogo na kushindwa kumudu familia zao.
Ameongeza kwa kusema kuwa  shirika la Mkuhumi umeanzisha rasmi shamba Darasa tangu Mwaka 2010 katika vijiji 8 Wilaya ya Kilosa na kwamba kila Kijiji  kuna vikundi viwili vinavyotekeleza mradi wa shamba darasa na kwamba wameanzisha mfumo wa kutoa zawadi kwa kila kikundi kinachofanya vizuri na mkulima mmoja mmoja kama motisha ili waweze kufanya vizuri.
Katika sherehe hizo ambapo mgeni rasmi alikuwa Mwenyekiti wa Halmashauri wilaya ya Kilosa Amer Mubarak ameweza kukabidhi zawadi kwa mshindi wa kwanza hadi wa tatu pamoja na kikundi ambapo mshindi wa kwanza alikuwa Tamasha Mkwechi amezawadiwa fedha taslimu elfu thelathini,Agripina Pweleza elfu 25 na Emili Mgabe shilingi elfu 15 na kikundi kimepata baiskeli aina ya foneksi na shilingi elfu 50.
Aidha akizungumza kwa niaba ya wakulima wa shamba Darasa katika Kitongoji cha Manyomvi Bi Tamasha Pweleza amesema kuwa wanaushukuru mradi wa Mkuhumi kwa kutoa mafunzo hayo na kwamba wananchi   wameweza kufuatilia kwa kina na wameiomba serikali itoe mikopo ya pembejeo kwa wakulima hao ili waweze kuendeleza kilimo.

No comments:

Post a Comment